Tag: Swahili

  • Faraka

    Sikujaliwa na moyo wa chuma
    Kuhimili yako mahaba na maumivu
    Kanichoma, mtima waniuma
    Tele, roho yangu imejaa maumivu
    Maisha yamenikwisha yake hamu
    Kanitia karaha moyoni mwangu
    Usoni mwangu sinayo tena tabasamu
    Nashindwa kukuita tena mpenzi wangu
    Tazamio langu nilidhani tatizo marafiki
    Wachochezi wenye hulka za kinafiki
    Kumbe yote ni wewe, kunguru na mwewe
    Asali nilipenda, kaona heri kuchonga mzinga
    Hakika nyuki kumfuga sharti ukubali na kuumwa
    Maumivu chungu nzima nashindwa kuvumilia
    Hisia mfarakano, moyoni nalia

    Penhive ✍🏾

  • Kukuacha Nitaanzaje?

    Una urembo kama hurlaini wa peponi
    Hisia zangu wazitia motoni
    Kila usiku u mwangu ndotoni.
    Macho yako mazuri
    Umbo lako nane namba
    Unanukia uturi
    Una Sauti kama kasuku
    Na nyodo kama vifungo
    Ni mwenye hakika huba
    Mahaba moyoni yamenikaba
    Penzi moto zaidi ya jua
    Wewe umeniridhi wengine wote pangua
    Napenda ulivyo, mso maringo
    Mahaba ndo langu kuu lengo
    Nakupenda, dhambi kusema uongo

  • Shubiri

    Ni wengi yamewaliza,
    Wengine yamewaliwaza,
    Yanacho kiza,
    Yanao pia mwangaza,
    Tamu kama pizza,
    Katu mja huwezi mkataza,
    Yana uchungu mate kumiza
    Yana utamu wake, roho kufaza
    Yana visasi,kulipiza
    Kiungulia,hisia kukata ja mashaza
    Akili sanasana kuwaza
    Furaha moyoni kujaza
    Yanayo taharuki ya giza
    Mja hali kumchakaza
    Hali yake kuwazawaza
    Nafsi kufurahi,nafsi kukwaza
    Ila sana hupendeza
    Moyo kudekeza…
    Nasisitiza
    Ni wengi yamewaliza
    Wengine yamewaliwaza

  • Taradadi

    Umeukwachu wangu moyo
    Sasa mwenzio nina choyo
    Mapenzi yamenifanya boyo
    Nayo nafsi kaufuata moyo
    Nizungushe angani kama pia
    Maana kwako ndiko nakwamia
    Maneno mengi utayasikia
    Chunga wasije kuharibia

  • Moyo Wangu

    Moyo wangu sio mpira, mateke kuupigapiga
    Usinipakulie zako hasira, mie sio yako tiba wala kinga
    Ilikushinda subira, ombi langu ukalipingapinga
    Kwa nilivokutumainia, ukaonelea bora kutangatanga

    Moyo wangu sio danganyadanganya, umechoka kuhanywahanywa
    Huba langu aminifu, na wengine Sitaki kuchanganywachanganywa
    Moyo wangu hupenda kikamilifu, hata ukinyanyaswanyanyaswa
    Moyo wangu mzinga wa asali kuugundua, kuila nyuki watakusumbua

    Moyo wangu ni harusi, moyo wangu ni matanga
    Nkikuzawadi ni kama harusi, sipoutunza ni yako majanga
    Moyo wangu una wake weusi, moyo wangu una wake mwanga
    Moyo wangu thamani, katu siupeani kihubahuba tena asilani…

Design a site like this with WordPress.com
Get started